MIAKA MIWILI TANGU KIFO CHA GEORGE FLOYD: Namna kifo chake kilivyomfanya kuwa alama ya mapambano dhidi ya mauwaji na ubaguzi wa rangi.

Mei 25, 2020, miaka miwili iliyopita, majira ya saa mbili usiku George Perry Floyd Jnr, alinunua pakiti la sigara katika duka linaloitwa Cup Foods katika makutano ya mtaa wa 38 wa Mashariki na mtaa wa Chicago kule Minneapolis, Marekani. Mwajiriwa wa duka lile alimshutumu Floyd kuwa alinunua pakiti lile la sigara kwa noti feki ya $20 na kuamua kumripoti. Baada ya maafisa wa polisi kufika eneo la tukio, walimtia mbaroni Bw. Floyd na kuifunga mikono yake nyuma kwa pingu, kumsogeza kando ya gari lao walipomlaza chini kabla ya afisa mmoja kuamua kumkandamiza shingoni kwa kutumia goti lake mpaka mauti ilipomfika.

George Floyd ni moja kati ya mamia, pengine maelfu ya watu waliouwawa kikatili kutokana na ubaguzi wa rangi (racism and white supremacy). Tofauti kubwa ni kwamba, muhanga wa safari hii katika mauwaji ya kikatili yanayosababishwa na dhana za kibaguzi, aliuwawa kikatili huku video iliyoonyesha mauwaji hayo kuanzia alipokamatwa mpaka kifo chake ikizua hisia za huzuni na mshtuko kwa watu duniani kote. Video hii ilirekodiwa na binti wa miaka 17 aitwaye Darnella Frazier kwa simu yake ya mkononi na baadaye kusambaa mtandaoni. Mauwaji haya yalizua taharuki na kuleta hamasa zaidi kwa muendelezo wa kauli mbiu maarufu ya kupinga unyanyasaji na ukosefu wa usawa kati ya watu wenye ngozi ya rangi nyeusi na nyeupe ambayo inafahamika kama ‘Black Lives Matter’ iliyoanzishwa na mabinti watatu baada ya mauwaji mengine ya kikatili ya kijana wa miaka 17, Trayvon Martin aliyepigwa risasi na jirani yao, George Zimmerman. Mbali na mchango mkubwa wa mitandao ya kijamii katika kuamsha hisia za watu na utambuzi juu ya ukatili wa polisi kwa Wamarekani weusi, uuwaji wa George Floyd pia ulikua wa kikatili sana. Askari polisi aliyesababisha kifo chake alimkandamiza shingoni kwa muda usiopungua dakika 8 na sekunde 46 huku Floyd akihangaika sana na kusema “siwezi kupumua” mara 16. Licha ya George Floyd kulalamika sana, afisa aliendelea kumkandamiza mpaka alipopoteza uhai wake. Uchunguzi zaidi uliofanywa na daktari wa kituo cha matibabu cha Hennepin ambako George Floyd aliwahishwa haukubainisha ushahidi wowote wa shinikizo la kubanwa kifua au kunyongwa hivyo pengine vichocheo fulani katika mfumo wake na kukandamizwa na afisa kulichangia kifo chake iliripoti BBC.

Moja kati ya kanuni za msingi ambazo zinalijenga taifa la Marekani ni pamoja na haki, usawa na uhuru wa kujieleza lakini kwa vizazi vingi sasa Wamarekani weusi wamekuwa wakihisi ukosefu wa usawa (wakionewa) huku hali hii ikiwafanya wakumbuke kipindi cha ukatili wa kitumwa. Badala ya kuangaliwa kwa uhalisia na hoja stahiki za kihistoria, wazawa wa Afrika na watu wenye ngozi nyeusi wameelezewa kwa mtazamo wa kimashariki zaidi ambao hutizama Waafrika au watu wenye asili ya Afrika kama walimbukeni, waliokosa elimu, wasiostarabika, masikini, tegemezi na wavamizi. Ni jambo linalostaajabisha wengi kuwa watu walioleta watumwa kutoka nyumbani kwao pa asili, wakaishi katikati yao (japo kama watumwa) na kuzaliana nao, leo wanawabagua na kuwaona wavamizi.

Tangu miaka ya 1960 kumekuwa na madai mengi ya haki na usawa nchini marekani kwa watu Weusi. Mwaka 1991 Rodney King, pia Mmarekan mweusi alipigwa kikatili na maafisa wa polisi wa Los Angeles baada ya kukamatwa sababu ya uendeshaji wa kasi. Mwezi Julai 2014 baba wa watoto 6 Eric Garner pia alifanyiwa ukatili na askari polisi uliosababisha kifo chake baada ya kutuhumiwa kuuza sigara moja kutoka kwa pakiti bila stempu za ushuru.  Mauwaji haya yote yalileta na yanaendelea kuleta taharuki huku waandamanaji mbalimbali pia wakikamatwa na kufungwa kutokana na vurugu kusemwa ‘zimepitiliza’ na mamlaka husika katika nyakati tofautitofauti. Mbali zaidi, baadhi ya waandishi wa habari pia wamekuwa wakikamatwa ilihali wakiwa wanajaribu tu kuionyesha dunia yale yanayoendelea. Watu mashuhuri kama Malcom X na Martin Luther King waliodai haki na usawa kutoka kwa ndugu ambao wanatofautiana tu rangi ya ngozi waliuwawa katika kutetea usawa huu.

Derek Chauvin, askari aliyesababisha kifo cha George Floyd alihukumiwa miaka 22 na miezi 6 jela, Juni 26, 2021 kwa mauwaji ya shahada ya pili na mashtaka mengine huku jaji akisema kuwa hukumu yake imetokana pia na unyanyasaji wake, matumizi mabaya ya wadhifa, na vilevile ukatili alioonesha kwa Floyd. Inadaiwa Chauvin alikwishalalamikiwa zaidi ya mara 12 katika muda wake wote wa uzoefu wa kazi kwa zaidi ya miaka 18 kuhusu kukiuka taratibu za kazi yake, iliripoti SkyNews katika Makala yake ya ‘8 Minutes and 46 Seconds - The Killing of George Floyd’. Mama wa Derek Chauvin, Carolyn Pawlenty alisema mahakamani kuwa, “Daima ninaamini kuwa huna hatia na sitabadili mtazamo wangu.” Askari polisi wengine watatu waliohusika na tukio la mauwaji ya George Floyd walikutwa na hatia ya makosa ya unyanyasaji na kusaidia mauwaji ya shahada ya pili.

Kumekuwa na wasiwasi kuwa huenda mzunguko na marudio ya matatizo yote haya ya unyanyasaji na mauwaji yanayofanywa na askari polisi dhidi ya Wamarekani weusi hauna mwisho. Wengi hudhani kuwa biashara ya utumwa ndiyo dhambi asilia iliyosababisha karne nyingi za mateso na ukosefu wa usawa kwa Wamarekani Weusi; ikiwa kuna ukweli wowote katika hili, basi watu hawa wanateseka kwa makosa ambayo hawakuyafanya. Kwa muda sasa, yaonekana kuwa kupata suluhu, ufumbuzi au njia thabiti za kudhibiti makosa haya ya ubaguzi wa rangi yaliyoenda mbali zaidi na kufikia hatua ya kuuwawa kwa raia wasio na hatia imeshindikana. Baada ya mauwaji ya George Floyd, watu wengi walishauri kuwa ufike wakati ambao askari polisi watanyang’anywa nguvu na vyeo walivonavyo ndipo masuala ya ukatili dhidi ya watu wenye ngozi nyeusi utaisha. Hata hivyo, meya wa Minneapolis wakati ule wa mauwaji ya George Floyd alisema kuwa itakuwa ngumu kuondoa kabisa polisi ambao kazi yao ni kulinda raia na mali zao lakini ilikuwa dhahiri kuwa mabadiliko katika jeshi la polisi yanahitajika.

Safari ya ubaguzi wa rangi imekuwa ni ndefu. Mpaka kufika sasa, wakati wa utandawazi, wakati ambao watu wengi wameelimika na kupata utashi wa kutosha kustaarabika na kutambua haki za binadamu ambazo hazibagui na hazichagui, ni jambo la kushangaza kuona watu wanabaguana na kuuana kwa sababu tu rangi za ngozi zao zinatofautiana. Kulikuwa na wakati ambao watu weusi nchini Marekani waliishi kwa hofu katika nchi hiyohiyo ambayo wao ni wazawa na pengine hadi sasa, baadhi wana hofu hiyo; nyakati ambazo mauwaji yangetokea na yasingeripotiwa sehemu yoyote wala kufahamika kwa watu. Kifo cha George Floyd, aliyekuwa baba wa watoto watano, kimekuwa kichocheo, jiwe kuu la pembeni katika kujenga dunia na kuleta mwamko na pengine mwanzo wa ukingo wa kuelekea kuondokana na tatizo hili. Aidha, matumaini kama haya yalishakuwepo awali; mfano mwaka 2009 baada ya nchi ya Marekani kupata rais wa kwanza mweusi, wengi walidhani huenda walishaona mateso ya mwisho ya aina hii kwa Wamarekani weusi lakini mauwaji haya yaliendelea kutokea. Licha ya ishara zote kuwa dunia inaenda katika uelekeo sahihi hasa baada ya mauwaji yan George Floyd kuonekana wazi, bado mwisho rasmi wa mauwaji na ubaguzi huu uko zaidi ya upeo wa macho na hata utabiri. Hata hivyo, kifo cha George Floyd kitabaki kuwa alama katika mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi. Chaguzi ingekuwa kwa dunia, basi hakika dunia ingechagua George Floyd aendelee kuishi maisha yake kwa amani, kuwalea watoto wake na kutimiza kikamilifu yale ambayo hakutimiza. Kama ni alama ya mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi na ukatili wa polisi, basi ingetafutwa alama nyingine. Lakini yaliyotokea yametokea; apumzike kwa amani, George Perry Floyd Jnr.


Comments

  1. Kunyanyaswa kwa Watu Weusi nchini Marekani ni mkakati wa kimfumo ambao umekuwapo
    kwa miaka mingi ukiwa na lengo la kuhakikisha hawapati fursa maridhawa sawia na Wazungu hivi kwamba nao wakaweza kuwa jamii yenye ustawi mujarabu - kimsingi, ni kama bado vidonda vyao vya utumwa vikiwa vinatoneshwa!

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

MFUMUKO WA BEI YA MAFUTA: Namna vita ya Urusi na Ukraine inavyochangia kupanda kwa bei ya mafuta na hatua zinazochukuliwa na serikali kukabiliana na mfumuko huo nchini Tanzania.

Ugonjwa wa 'Monkeypox': Je, tunapaswa kuwa na wasiwasi?

MALKIA ELIZABETH II